USIRI WA ELIMU YA UZAZI WACHANGIA MIMBA ZA UTOTONI



Kwa ufupi

Wazazi wanahofia kuongea na watoto masuala yanayohusu uzazi.

Kitendo cha jamii kutowaweka wazi vijana kuhusu elimu ya uzazi kimetajwa kuwa sababu inayochangia kuendelea kuwepo tatizo la mimba katika umri mdogo na mimba zisizotarajiwa kwa wanafunzi wa vyuo.

Mkurugenzi wa Chama cha Madaktari Wanawake (Mewata), Dk Joyce Lyimo amesema hayo wakati wa tathmini ya mradi wa elimu ya uzazi kwa vijana uliotekelezwa mkoani Iringa chini ya ufadhili wa mfuko wa asasi za kiraia.

Dk Joyce amesema wamebaini kuna vijana walio vyuoni lakini hawafahamu kwa kina kuhusu afya ya uzazi.

“Unaweza kushangaa ni kwa nini vijana wengi wa kike wakiwa chuo wanapata ujauzito, si wote wanakuwa wamepanga kufanya hivyo wapo ambao wamejikuta katika hali hiyo kwa sababu walifanya mapenzi yasiyo salama,” amesema.

Dk Joyce amesema, “Kwa wale ambao wapo bado shule za msingi na sekondari, tumebaini walikuwa hawapati elimu. Wazazi bado wanahofia kuongea na watoto wao masuala yanayohusu uzazi,” amesema.

Kupitia mradi huo, amesema waliwafundisha vijana mbinu za kukabiliana na hali hiyo na matokeo chanya yameanza kuonekana mkoani humo.

Meneja wa fedha na uendeshaji, John Aswile amesema miradi mitano ilipata ufadhili wa mwaka mmoja kupitia asasi ya Piscca iliyo chini ya Serikali ya Ufaransa.

     

0 Comments