MKANGANYIKO HUU NANYI MNAUONA?


Humphrey Polepole 

Kwa ufupi
Utagundua misingi hii niliyotaja inaruhusu wananchi kuendelea kujadiliana mpaka wakiwa kwenye mstari wa kwenda kupiga kura. Mijadala ni jambo la afya katika jamii yoyote ile iliyoendelea.


Wahenga walisema anayeshindana na wakati atagonga ukuta
Wiki hii napenda kuzungumzia suala ambalo mara zote watu wasio na nia njema hupenda kumrejea ndivyo sivyo rais wetu mpendwa na naona hii imekuwa desturi siku hizi. Mara kadhaa akizungumza, utaona siku zinazofuata watu wametohoa alichokisema mkuu wa nchi na mara nyingi huwa wametohoa ili kukidhi matakwa na masilahi yao. Hii siyo sawa.
Mkuu wa nchi alikwenda kwenye Bunge Maalumu akazungumza wengine wakadiriki kusema mkuu ameshatoa maelekezo, hata yeye mwenyewe alikuja kufafanua baadaye alichokifanya kwenye Bunge Maalumu na kwamba hakuwahi kutoa maelekezo.
Hata alipotutangazia kuwa na mchakato wa kupata Katiba Mpya, watu wale wenye hila hawakusita wakaenda mbali zaidi ya kutohoa maneno yake na hata kudiriki kumhoji na kuhoji uhalali wa uamuzi wake.
Unajua utovu wa nidhamu siyo suala la rika, ni suala la mtu binafsi au mtoto, kijana, mtu wa makamo au mzee. Kutohoa, kutafsiri na kupindisha kauli za mkuu wetu wa nchi ni kiwango kikubwa cha utovu wa nidhamu, hasa inakuwa mbaya zaidi pale ambapo anayefanya utovu wa nidhamu ni mtu wa makamo.
Hawa vijana ni matokeo ya namna mnavyotulea, mara nyingi sisi vijana hupenda kujinasibu na tabia na mienendo ya wale wanaotupa hamasa.
Kama wewe ni mwizi basi ujue wale vijana wako watakuwa wameanza ku-“develop” tabia za wizi. Kama wewe ni mtu mshari tu tena ngumi mkononi, basi huna haja ya kuhoji ukisikia watu wamepigwa ama wamerushiwa viti. Ujue kwamba, ile tabia yako inafanya kazi ndani ya wale vijana wako. Wale vijana ambao wanapata hamasa kutoka kwa watu wenye uchu ya madaraka kwa hakika utaona hata lugha zao mitandaoni ni za kibabe. Mara nyingi ni za matusi, vijana hawa huwa hawana simile, hasa mijadala inapokuwa imesheheni watu wanaoshindanisha nguvu za hoja. Punde wao hubadili kibao na kushindanisha hoja za nguvu na huwa hawana aibu. Nasikia hawa wanaweza hata kulipwa kufanya lolote. Hii ni shida tunaitengeneza leo na itakuja kutusumbua baadaye miaka kadhaa ijayo, Mwenyezi Mungu atupe umri na afya tutashuhudia.
Tofauti kati ya kampeni na elimu ya uraia
Nieleze bayana kwamba mchakato wa kuandika Katiba Mpya, unapaswa kuwa mchakato ambao wananchi wanashiriki kwa kiwango cha juu kabisa. Kimsingi wataalamu wa Katiba wanaainisha misingi mikubwa minne ambayo ni lazima izingatiwe pale nchi inapokuwa inaandika Katiba yake. (i)Public Participation yaani ushiriki wa watu, (ii) Inclusiveness (including gender equity) and representation yaani ujumuishi unaoheshimu dhana ya nafasi na usawa wa kijinsia pamoja na uwakilishi, (iii) Transparency yaani uwazi na (iv) ni National ownership yaani umiliki wa mchakato kitaifa.
Utagundua misingi hii niliyotaja inaruhusu wananchi kuendelea kujadiliana mpaka wakiwa kwenye mstari wa kwenda kupiga kura. Mijadala ni jambo la afya katika jamii yoyote ile iliyoendelea. Ni lazima watu wazungumze, wagonganishe mawazo yao kwa hoja na sababu na ni katika mchakato huu wa kujadiliana, ndipo uelewa mpana hujengwa na kusimikwa katika fikra za watu.
Watu wanapokuwa wameelimika basi mara zote huweza kufanya uamuzi sahihi. Hii ndiyo inaitwa elimu ya uraia juu ya mchakato wa kupata Katiba Mpya pamoja na maudhui yake. Tukizungumza maudhui ya mchakato huu ni pamoja na Katiba ya Mwaka 1977 inayotumika sasa, Rasimu Toleo la Awali, Rasimu Toleo la Pili pamoja na viambatisho vyote.
Watu wana haki ya kueleweshwa juu ya mambo haya. Mimi bibi yangu umri wake umekwenda sana, nadhani anafika miaka 100 na hajui kusoma wala kuandika, lakini haki ya kupiga kura anayo. Hivi, unadhani mimi nitamwacha Tumwihukage Semwenga au kama wajukuu tunavyomwita “Bibi Nundu”, aende akapige Kura ya Maoni pasina kuwa nimemsomesha?
Hivi unadhani nitamwacha Bibi Nundu abaki mweupe juu ya mchakato hadi kampeni zitakapoanza?
Kwanza hatonielewa hata kidogo. Ni hili ndilo ninalolimaanisha kwamba, elimu ya uraia ni lazima hasa ikizingatiwa kuwa hakuna chombo chochote cha kisheria au cha kikatiba ambacho kina dhamana ya kutoa elimu ya uraia. Basi ni budi tuelimishane zaidi na zaidi kwa kadri muda utakavyoturuhusu. Ujumbe huu ni kwa faida ya bibi na babu wote nchini ambao wangependa kuona tuna Katiba Mpya inayojengwa katika ushiriki wa watu.
Elimu ya Uraia siyo Kampeni ya Kura ya Maoni hata kidogo, bali ni nafasi yetu adhimu na adimu kulielewa taifa letu na kuuelewa mchakato huu wa kihistoria kama mwananchi mmoja mmoja.
Katika jamii iliyoendelea huwa siyo ustaarabu kwa Serikali kuingilia zoezi la wananchi kuelimishana kwa hoja na sababu. Tungekuwa zile zinaitwa “nchi za wenzetu” basi Serikali ingetoa fungu ili watu wajadiliane kwa uwazi, kwa hoja na sababu, na siyo kuwa na mkakati wa kulazimisha watu kuelekea uamuzi ambao labda Serikali au upande fulani unapendelea.
Sisi tumestaarabika, hatufanyi mambo hayo ni vile tu hela huwa hazitoshi, lakini zingekuwepo nina uhakika Serikali yetu sikivu ingelitenga fungu kupitia mfuko ule wa utawala bora, ili watu waendeshe midahalo nchi nzima.
Tume Huru ya Uchaguzi ni kwa shughuli ipi?
Hapa nina swali la msingi sana, nilisikia hii hoja ya Tume Huru ya Uchaguzi ilianza tangu Uchaguzi Mkuu wa Kwanza wa Rais, Wabunge na Madiwani katika mfumo wa vyama vingi katika Jamhuri yetu ya Tanzania mwaka 1995. Suala hili limeendelea kujirudia mwaka 2000, 2005, 2010 na bado ni jambo ambalo ni kana kwamba tumeshakubaliana kwamba chaguzi zinazokuja lazima zisimamiwe na Tume Huru ya Uchaguzi.
Sasa jana nilifanya tafakuri ile ambayo angalau mara tatu kwa wiki hufanya, nikajiuliza hivi Uchaguzi Mkuu wa 2015 na Kura ya Maoni lipi zoezi muhimu kuliko lingine? Kwa akili zangu nikasema Kura ya Maoni ni suala la kuandika na kuweka uhalali wa Katiba Mpya ya nchi, Sheria Kuu ya Nchi, Mkataba Mpya kati ya Viongozi na Wananchi ambayo kwa hiyo mambo mengi hufuata, hutokea na kupata uhalali ukiwemo Uchaguzi Mkuu.
Baada ya hoja na sababu hizo nikasema basi Kura ya Maoni ni muhimu zaidi kuliko Uchaguzi Mkuu na kwa maana hiyo, kama tungehitaji Tume Huru ya Uchaguzi, basi ingekuwa ni katika ngazi ya Kura ya Maoni kwanza. Sasa niwaulize; hivi katika mijadala inayoendelea umewasikia Watanzania wakikumbusha juu ya uwepo wa Tume Huru ya Uchaguzi itakayosimamia Kura ya Maoni? Au wale wapiga chapuo wa kidesturi kwa uwepo wa Tume Huru ya Uchaguzi mbona siwasikii mkilizungumzia hili? Au kimya chenu ni masilahi katika hili?
Marekebisho ya 15 lini?
Sasa yale makubaliano kati ya Mheshimiwa Rais na Kituo cha Katiba Tanzania (TCD) kwamba tutafanya marekebisho madogo “minimum amendments” ya Kumi na Tano kwa Katiba ya Mwaka 1977 ili ikidhi takwa la Tume Huru ya Uchaguzi, Ushindi wa Uchaguzi wa Rais wa zaidi ya Asilimia 50, Kuhoji Matokeo ya Uchaguzi wa Rais pamoja na suala la Mgombea Huru, yatafanyika lini?
Tuko Novemba na Bunge la Novemba linaendelea na sijasikia Muswada wa Marekebisho ya Katiba. Na ikumbukwe haitakuwa busara hata kidogo kuupeleka Muswada wa Marekebisho ya Katiba ya Mwaka 1977 kwa Hati ya Dharura au kama inavyojulikana kwa Kiingereza “Certificate of Urgency”.
Napenda ieleweke kwamba, miswada inayopelekwa kwa hati ya dharua huwa kwa kiasi kikubwa inaminya haki ya wananchi kushiriki kikamilifu katika utengenezwaji wa miswada hiyo.
Je, ratiba inaruhusu?
Kwa kweli baada ya kukokotoa hesabu za wakati naona changamoto ya wakati, tuna kikao cha Bunge mwezi Januari-Februari, kabla ya kwenda katika Kura ya Maoni. Kura ya Maoni itakuwa Aprili 30, ambayo itakuwa imetanguliwa na zoezi zito la kampeni za Kura ya Maoni na tuseme matokeo yake yatajulikana ndani ya wiki mbili za kwanza za mwezi Mei.
Ikumbukwe kwamba, itakuwa kipindi hicho ambacho kinyang’anyiro cha wagombea urais katika ngazi ya vyama ndiyo itakuwa joto juu. Kikao cha Pili cha Bunge kitakuwa Julai-Agosti, kikao cha Bajeti na ni wakati huo rais anapaswa kulivunja Bunge ili baada ya hapo tuelekee kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu.
Ukisoma nami kwa umakini, utaona kuna tatizo, sielewi kwa nini tumeamua kutumia Mwendokasi wa Mwanga, sina tatizo na Mwendokasi, lakini je, tumejipanga vizuri kuendana na mwendokasi ilhali tukijua vyombo, taasisi, mifumo, taratibu, kanuni na wenye dhamana ya kutusaidia katika baadhi ya mazoezi mazito kama Kura ya Maoni hatutakuwa tumeweza kuviunda na kuvianzisha kabla ya matuko na hatua stahiki kufikiwa?
Hivi ni mimi tu au na wewe msomaji unaliona hili, kama umeliona zungumza na mwenzako na mjadiliane kwa hoja na sababu. Nawahakikishia mtakuwa mnafanya kazi njema kwa nchi yenu, nchi yetu hii inayoitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo ndani yake watoto wenu na wajukuu wenu wataishi raha mustarehe iwapo mtachukua hatua sasa.
Itaendelea wiki ijayo

0 Comments