Kwa ufupi
Hata hivyo, baadhi ya wanaharakati wanasema idadi
kubwa ya Watanzania hususan kundi la vijana, wamekuwa ni wavivu wa
kujituma, kufikiria mbinu na kutumia fursa zilizopo.
Miaka mitano iliyopita, kundi la Watanzania
wasiokuwa na ajira limezidi kuongezeka, huku sekta ya umma na binafsi
zikishindwa kuhimili wingi wa watu hao, hivyo kuwachukua wachache.
Hata hivyo, baadhi ya wanaharakati wanasema idadi
kubwa ya Watanzania hususan kundi la vijana, wamekuwa ni wavivu wa
kujituma, kufikiria mbinu na kutumia fursa zilizopo.
Katika kudhihirisha ukubwa wa tatizo hilo, Waziri
wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka akiwa bungeni mwaka jana alinukuliwa
akisema taifa lina uwezo wa kukidhi mahitaji ya ajira 80,000 mpaka
100,000 kwa mwaka ukilinganisha na mzigo wa vijana 400,000 hadi milioni
moja wanaoingia kwenye soko la ajira kila mwaka.
Kutokana na mazingira hayo, Watanzania wawili
ambao ni Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Lutherani usharika wa Matumbi,
Christosiler Kalata na Mhadhiri wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es
Salaam (Duce), Emmanuel Kwayu, wanazindua kitabu kipya kiitwacho
‘Ukombozi wa Fikra’.
Maudhui ya kitabu hicho yanayolenga kurejesha tumaini la vijana waliokata tamaa na kufungua ukurasa mpya wa maisha.
Kinaeleza: “Uamuzi wako ndiyo unaweza kukuimarisha
au kukudhoofisha. Ubora wa uamuzi wako unategemea ubora wa nafasi yako.
Usikate tamaa na hatua sahihi za kuamua katika mazingira uliyo nayo kwa
sasa.”
Mchungaji Kalata anasema hatua hiyo inatokana na
ongezeko la vijana wengi wanaoyumbishwa kifikra na wanasiasa, imani
potofu za ushirikina na rushwa.
Mchungaji Kalata ambaye ni mwandishi wa kitabu
hicho na Mlezi wa Jukwaa la Amani kwa vijana wa Kiislamu na Kikristo
nchini, anasema ukombozi wa fikra unahitajika ili kubadili maisha na
tabia za Watanzania.
“Usomaji wa vitabu ni taswira mpya yenye majibu ya
maswali magumu ya Watanzania waliokata tamaa na wasiokuwa na mbadala,”
anasema.
Hali ilivyo kwa sasa
Hali ya ilivyo kwa sasa katika maisha ya Watanzania inazidi kuwa tishio, licha ya kuwapo kwa taarifa za kukua kwa uchumi nchini.
Mtandao wa Afrobarometer, chini ya taasisi ya
utafiti ya Repoa, imetoa matokeo ya utafiti wa awamu ya sita ulioonyesha
hali ya uchumi kwa Watanzania ni mbaya zaidi kuliko miaka kumi
iliyopita.
Utafiti huo ulifanyika kati ya Oktoba na Septemba mwaka jana
huku ukihoji Watanzania 2,386. Dk Lucas Katera kutoka Repoa anasema;
“Mwaka 2003, asilimia 42 walisema hali ya uchumi ni mbaya, mwaka 2005
asilimia 38, mwaka 2008 asilimia 57, mwaka 2012 asilimia 72 na mwaka
jana asilimia 67 walisema hali ni mbaya ya uchumi.”
Pamoja na mazingira hayo, Katibu Mkuu wa Chama cha
Wafanyakazi nchini (Tucta), Nicholaus Mgaya anasema Serikali imekuwa
ikifungua fursa na kuzifunga yenyewe.
Anasema vijana wengi waliotambua baadhi ya fursa
na kuzitumia katika mazingira yanayowazunguka, wamekuwa wakikutana na
vikwazo vinavyokatisha tamaa.
Mgaya anasema sera ya ajira nchini inaonekana
kukinzana na sera ya biashara kutokana na vikwazo vinavyoendelea
kujitokeza kwenye baadhi ya sekta.
Mgaya anasema suala la kujikomboa kifikra kwa
Mtanzania lazima lijitokeze kwa kila mmoja kutokana na uhitaji wa huduma
za kijamii vinginevyo hataweza kuishi salama.
“Mfano, halmashauri nyingi sana zina upungufu wa
wataalamu wa mifugo, kilimo na afya lakini imeshindwa kuwapatia ajira
vijana waliomaliza vyuo vikuu. Wengi wanahangaika mitaani. Kwa hivyo
sehemu kubwa ya ukombozi wa kifikra inategemea mchango wa Serikali.”
Ukali wa maisha utakwisha?
Pamoja na vikwazo hivyo, Mhadhiri wa Chuo Kikuu
Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (Duce), Emmanuel Kwayu anasema ukali
wa maisha hapa nchini unaweza kupungua kwa kiwango kikubwa endapo
Watanzania watabadili mwenendo na kasi ya utumiaji wa fursa
zinazowazunguka katika mazingira yao.
Anasema fursa zinaweza kuwapo kwenye mazingira ya
jamii lakini watu wake wakabakia kuwa maskini endapo hawatafungua fikra
zao. Anatoa mfano juu ya umuhimu wa usomaji wa vitabu akisema:
“Kwanza, kila mtu anahitaji kuhoji kusudi lake la
kuzaliwa hapa duniani. Hakuna aliyezaliwa kwa bahati mbaya. Ukishafahamu
sababu ya kuwapo kwako, jambo la pili lazima ujue msingi wa maswali na
majibu ya umaskini kwa Mtanzania. Matokeo ya maisha yako ya sasa ni
msingi wa maandalizi yako ya jana,” anasema na kuongeza:
“Pia, Mtanzania anatakiwa kufungua ufahamu wa
kutambua ni kiongozi gani anayeweza kumfaa, hususan tunapoelekea kwenye
Uchaguzi Mkuu. Siyo suala la kuyumbishwa na fikra za wanasiasa, siyo
kuamuliwa, unatakiwa kuchambua na kutafsiri mahitaji ya sasa kwako.”
Hii ni kusema Watanzania wanahitaji elimu zaidi ili iwafumbue macho waweze kuzitumia kikamilifu fursa zilizopo nchini.
Pamoja na ufafanuzi wa wasomi hao, mambo muhimu yanahitaji
kuzingatiwa. Serikali inapaswa kumwezesha Mtanzania maskini kujikomboa
na umaskini kupitia vikwazo mbalimbali vinavyowakwamisha wakulima na
wajasiliamali.
Ni muhimu pia kuanzisha elimu ya ziada kwa
wanafunzi wa vyuo vikuu, itakayomsaidia kujitambua, kutambua mazingira
yanayomzunguka na jinsi gani anaweza kuzitumia fursa zilizopo, bila
kufikiria mitazamo ya kuajiriwa kila wanapomaliza masomo.
Vijana wanapaswa kuhamasishwa kujenga utamaduni wa kufanya kazi yeyote bila kuona aibu na kuwa na juhudi ili wafanikiwe.
0 Comments