MATESO NILIYOPITIA MIAKA 22 - SAMSON MAGOTI

Aliyekuwa mfanyakazi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Samson Magoti akizungumza na waandishi wa Mwananchi nyumbani kwake Yombo Dovya jijini Dar es Salaam jana. Picha na Edwin Mjwahuzi

Kwa Ufupi

Hatimaye haki hiyo imepatikana Oktoba 2 mwaka huu baada ya Mahakama ya Rufani kuwarejesha ikisema walifukuzwa kazi mwaka 1993 bila kufuata sheria.

Dar es Salaam. Haikuwa kazi rahisi. Miaka 22 ya wafanyakazi 31 wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kutafuta haki yao iligubikwa na umaskini, maradhi na vuta nikuvute ya migogoro ya kisheria.

Hatimaye haki hiyo imepatikana Oktoba 2 mwaka huu baada ya Mahakama ya Rufani kuwarejesha ikisema walifukuzwa kazi mwaka 1993 bila kufuata sheria.

Kiongozi wa wafanyakazi hao, Samson Magoti aliyesimama kidete kuhakikisha wanapata haki yao, amezungumza na Mwananchi na kueleza maisha magumu aliyopitia katika kipindi hicho ikiwamo kuugua kiharusi kutokana na mawazo na kukimbiwa na mke.

“Haikuwa kazi rahisi, lakini hatimaye Mahakama imetenda haki na kama si majaji wanaosimamia maadili ya kazi yao, leo pengine tusingepata haki yetu,” alisema Magoti.

Mazungumzo haya na Magoti yalifanyika nyumbani kwake, Yombo Dovya, wilayani Temeke tulipomkuta yeye na familia yake ya watoto wanne kati ya sita, mke (mwingine) na mama yake mzazi, ajuza wa miaka 102.

Magoti, mrefu kiasi na mweusi, anakuja kutupokea akiwa ameambatana na watoto wake watatu, wadogo; Happy, Eliza na Witi.

Tulipofika nyumbani kwake, alitukaribisha kwenye banda la uani ambalo baadaye alitueleza kuwa lilikuwa likitumika kufugia kuku lakini kutokana na ugumu wa maisha, sasa ndiyo makazi ya familia hiyo.

Robo ya banda hilo imejengwa kwa matofali na robo tatu iliyosalia ni maboksi (ceiling board).

Tulipowasili nyumbani kwake, mke wa sasa wa Magoti, Naomi Samson alikuwa akijiandaa kwenda kuuza ufuta katika Shule ya Msingi Buguruni na alipotukaribisha, tuliuliza bei ya ufuta naye alitujibu: “Huu ni Sh100, una Bluetooth, Whatssap na Memory card.”

Baada ya kununua ufuta wa Sh500, tulianza mazungumzo yetu na Magoti ambaye alifukuzwa kazi Machi, 29, 1993.

“Nilikaa na mke wangu wa kwanza katika kipindi cha mwanzo tu wakati nina hela za mafao, baada ya hapo hali ilianza kubadilika naye akabadilika,” alisema.

Alisema miaka mitatu tu, baada ya kufukuzwa kazi, migogoro ilianza kwenye ndoa yake, mkewe alibadilika naye akawa hana sauti ndani ya nyumba.

“Kama huna kazi unakuwa mnyonge, huna sauti, kwa sababu kila unalomwambia atakujibu atakavyo na atasingizia anatafuta hela na wewe kweli huna.” Baada ya migogoro hiyo, mke wake aliondoka na kumuachia watoto watatu.

Nunua gazeti la Mwananchi leo ili uisome habari kamili, waweza kununua na kusoma gazeti hili kwa mtandao

0 Comments