AFISA MIKOPO, BODI YA ELIMU YA JUU ASIMAMISHWA KAZI

Kwa ufupi

Profesa Ndalichako amesema  imebainika ofisa huyo hakufanya uhakiki wa wanafunzi waliopewa mikopo.

Dar es Salaam. Waziri wa Elimu, Profesa Joyce Ndalichako amemsimamisha kazi ofisa mikopo wa Chuo Kikuu Ardhi, Rajabu Kipango kwa kushindwa kukamilisha mchakato wa kutoa mikopo kwa wanafunzi waliopatiwa mkopo licha ya Serikali kuwasilisha fedha kwa wakati.

Uamuzi huo umefikiwa baada ya wanafunzi  kulalamika kutoingiziwa mikopo na kusababisha kushindwa kujikimu.

Baada ya malalamiko hayo, imebainika ofisa huyo kutofanya uhakiki wa wanafunzi waliopewa mikopo, huku Serikali ilishatoa fedha kwa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB).

Profesa Ndalichako amesema leo Alhamisi Novemba 23,2017 kuwa, Serikali haiwezi kukwamishwa na watu wachache.

Ameagiza vyuo vingine kukamilisha mchakato wa mikopo ili kuondoa malalamiko ya wanafunzi kushindwa kupata fedha kwa wakati.

Pia, ameagiza wakuu wa vyuo vyote nchini kukaa na wanafunzi na kutatua matatizo yao badala yakukaa ofisini.

"Haingii akilini ofisa mikopo eti mwanafunzi anakufuata kazi yako ni kumzungusha badala ya kulifanyia kazi," amesema.

Profesa Ndalichako amesema kumekuwa na lawama kwa wanafunzi kwamba hawalipi ada kwa wakati, wakati Serikali ilishatuma fedha kwa ajili ya kuwapatia mikopo.

  

0 Comments