SHULE YA SEKONDARI PIUS MSEKWA IPEWE GARI- WAZIRI MKUU MAJALIWA


Waziri Mkuu Aagiza Sekondari Ya Pius Msekwa Ipewe Gari

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemtaka Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Ukerewe Bw. Frank Bahati awe amepeleka gari katika shule ya Sekondari ya bweni ya Pius Msekwa ifikapo Februari 25 mwaka huu.

Amesema shule hiyo yenye wanafunzi zaidi ya 700 lazima iwe na chombo cha usafiri kitakachotumika kwa ajili ya shughuli mbalimbali ikiwa ni pamoja na dharura za kuwapeleka hospitali wanafunzi pale wanapougua.

Waziri Mkuu alitoa agizo hilo jana (Jumapili, Februari 18, 2018) wakati alipotembelea shule hiyo na kuzindua madarasa na mabweni yaliyojengwa kupitia mradi wa Mpango wa Elimu wa lipa kulingana na Matokeo (EP4R).

“Wakurugenzi mnatakiwa kutambua shule hizi ni zenu, hivyo mnapaswa kuzihudumia. Shule hii inawafunzi zaidi ya 700 na wanalala hapa hapa hivyo lazima kuwe na gari la kuwahudumia wanafunzi hasa wakati wa dharura.”

Alisema Serikali haiwezi kuiacha shule hiyo bila ya kuwa na chombo cha usafiri, ambapo alimsisitiza Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kuhakikisha anatoa kipaumbele kwa taasisi za umma ili ziweze kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Hata hivyo, Waziri Mkuu aliwwagiza Wakurugenzi wote nchini kushirikiana na uongozi wa shule mbalimbali za Serikali katika kutatua baadhi ya changamoto zinazoikabili.

Miongoni mwa changamoto hizo ni malipo ya watumishi wasaidizi wakiwemo wapishi, walinzi na madereva, ambapo aliwataka wachukue jukumu la kuwalipa watumishi hao badala ya kuacha ya kuwaachia Wakuu wa Shule.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliziagiza halmashauri zote nchini kuhakikisha zinamalizia ujenzi wa vyumba vya maabara katika shule zao zilizobaki na Serikali itasambaza vifaa vya maabara mara zitakapokamilika.

Waziri Mkuu alisema tayari Serikali ilishasambaza vifaa vya maabara katika shule 1,696 za sekondari nchini ambazo zilikamilisha ujenzi.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU,

JUMATATU, FEBRUARI 19, 2018.

0 Comments