WALIMU 104 SEKONDARI WASHUSHWA SHULE ZA MSINGI, KILIMANJARO.


WALIMU 104 wa masomo ya sanaa kutoka shule za sekondari wamehamishiwa katika shule za msingi, ili kupunguza tatizo la upungufu wa walimu katika Halmashauri ya Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Chikira Mcharo amesema hayo jana wakati akijibu hoja ya Diwani wa kata ya Arusha Chini, Rojas Mmari wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani.

Amesema huo ni mpango wa serikali kutokana na tatizo la upungufu wa walimu 23,000 katika shule za msingi nchini, hivyo katika awamu ya kwanza, serikali imechukua walimu wa sekondari ambao hawakuwa na vipindi vingi huku ikiendelea na mkakati wa kumaliza tatizo hilo.

Mcharo alisema kati ya walimu hao waliohamishiwa shule za msingi mpaka sasa walimu 48 ndiyo walioripoti kwenye vituo vya kazi na kuwasilisha maombi ya malipo yao.

Diwani Mmari aliomba serikali kuangalia utaratibu huo kwa sababu walimu wanahamishwa kutoka sekondari kwenda shule za msingi zilipo kwenye kata hiyo hiyo wanaathirika kisaikolojia kwa sababu jamii inayowazunguka inawadharau na kuona kama wameshushwa vyeo.

Mcharo amesema, uhamisho huo hautawaathiri kisaikolojia kwasababu hawajashushwa vyeo na hauna athari yoyote katika maslahi yao ya kiutumishi.

Pia halmashauri iliwaandaa kisaikolojia kwa kuwaelimisha kuhusu mabadiliko hayo kabla ya kuwapa barua zao za uhamisho.

0 Comments