BRN YAITOA SHULE KUMI BORA KWENDA KUMI MBOVU

Mh Shukuru Kawambwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi
Kwa ufupi
Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Ufundi Iyunga ya jijini hapa, France Mung’ong’o alisema jana kuwa yeye pamoja na wafanyakazi wa shule yake wameshikwa na ganzi kutokana shule yake kuwa moja ya shule 10 za mwisho kwa matokeo mabaya.
 
 

Mbeya/Dar. Matokeo ya kidato cha sita yaliyotangazwa juzi na Baraza la Mitihani la Taifa (Necta), yamewashtua walimu wakuu wa shule za sekondari za Iyunga mkoani Mbeya na Tambaza jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Ufundi Iyunga ya jijini hapa, France Mung’ong’o alisema jana kuwa yeye pamoja na wafanyakazi wa shule yake wameshikwa na ganzi kutokana shule yake kuwa moja ya shule 10 za mwisho kwa matokeo mabaya.
“I’ m shocked (nimeshtushwa). Sikutarajia matokeo haya. Si mimi tu, hata walimu wenzangu hadi sasa hawaamini kwani kwenye mtihani wa mock (majaribio) ya kitaifa wanafunzi wangu walifanya vizuri na wa daraja la kwanza walipatikana wanafunzi 14 kipindi hicho,’’ alisema.
Alisema kutokana na hali hiyo, walimu jana walikuwa na vikao vya kiidara na leo wanatarajia kufanya mkutano wa pamoja kusaka sababu za kufanya vibaya.
Wanafunzi ambao sasa ni wa kidato cha sita walipoulizwa jana kuhusu habari hizo walijibu kwa sauti kubwa ‘mbayaaa’.
Kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa juzi Shule ya Sekondari ya Iyunga iliyoanza 1960, ni ya 262 kati ya sekondari 268 za aina yake kitaifa jambo lililoifanya iwe moja ya shule 10 za mwisho.
Akizungumza jana baada ya kuulizwa sababu za shule hiyo kufanya vibaya, Mng’ong’o alisema: “Nimeshikwa bumbuazi kutokana na ukweli kwamba nilikuwa nikiamini kwamba mwenendo wa kitaaluma unapanda.”
Hata hivyo alisema kero za jumla ambazo anahisi kuchangia ni upungufu wa walimu na wanafunzi wengi kurundikana kwenye darasa moja .
Alisema kwa kawaida shule yake ni ya mchepuo wa sayansi na kwamba ni makosa wanafunzi zaidi ya 100 kukaa chumba kimoja kufundishwa masomo ya Fizikia, Baiolojia na Kemia.
“Pia shule yangu ina upungufu wa walimu sita wa kidato cha tano na sita. Hivi sasa wapo walimu 11.
Mwalimu wa taaluma, Muhoja Bundala akitoa maoni yake alisema watakaa kuchambua sababu na kwamba hawatakubali kushika mkia mwakani.
Bundala aliwataka walimu na wanafunzi wa shule hiyo kuwa watulivu katika kipindi hiki wakati wakitafakari na kwamba kinachotakiwa ni kujipanga.Akizungumzia jana, mwalimu mkuu wa Shule ya Sekondari Tambaza, Hussein Mavumba alisema kuwa wameyapokea matokeo hayo kwa mshtuko mkubwa kwani halikuwa jambo walilokuwa wakilitarajia.
Mwalimu Mavumba alisema kuwa amewaita walimu na baadhi wa wakuu wa idara za masomo kuona nini kimetokea hata shule hiyo iliyokuwa maarufu kwa kufanya vizuri kushika nafasi 10 za mwisho.
“Nitakutana na walimu wangu na tutafanya tathmini za kisayansi kujua nini kilikosewa hadi kusababisha matokeo hayo,” alisema.
Baadhi ya wanafunzi walioomba kutokutajwa majina yao, waliidokeza Mwananchi kuwa uhaba wa walimu masomo ya sayansi ambayo ndio yameongoza kwa kufelisha zaidi shuleni hapo, upungufu wa vifaa vya maabara na uzembe wa wanafunzi wenyewe ni miongoni mwa sababu zilizochangia matokeo mabaya.
Shule ya Sekondari Tambaza imeshika nafasi ya tatu kutoka mwisho, matokeo mabaya zaidi yakilinganishwa na yale ya miaka minne iliyopita.
Imeandikwa na Lauden Mwambona na Mosha Mustapha, IJMC.

0 Comments