NANI ANAYEZUIA KATIBA MPYA?

  • CCM, Ukawa watupiana lawama

Nani anakwamisha upatikanaji wa Katiba Mpya? Ni swali lililokuwa likiongoza mdahalo wa Tanzania Tunayoitaka ambao uliandaliwa na Taasisi ya East African Business and Media Institute (EABMI) na kufanyika jijini Dar es Salaam.
Mdahalo huo uliitishwa kujibu swali hilo ambalo limekuwa likiulizwa na Watanzania wengi, hasa baada ya wabunge wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kususia mjadala wa Bunge la Katiba,  wakidai CCM inataka kujadili rasimu yao badala ya ile iliyowasilishwa kwenye bunge hilo na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Ukawa wamekuwa wakisisitiza kuwa  hawatarejea kwenye Bunge la Katiba linalotarajia kuanza Agosti 5, mwaka huu hadi watakapothibitishiwa kwamba majadiliano yatakuwa yakiihusu Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyokuwa ikiongozwa na Jaji Joseph Warioba.
Mdahalo huo ulikuwa ukiongozwa na Mwanyekiti Mtendaji wa EABMI, Rose Mwakitwange na uliwakutanisha wazungumzaji wakuu ambao ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Uhusiano na Uratibu, Stephen Wassira, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu na Profesa Ibrahim Lipumba.
Wazungumzaji hao walitoana jasho wakati wakijibu swali  hilo na mustakabali wa Mchakato wa Katiba, hasa kuhusu muundo wa muungano.
Profesa Lipumba anaanza kujibu swali hilo kwa kueleza kuwa wahafidhina wa CCM, ndiyo waliokwamisha upatikanaji wa Katiba Mpya. Anasema Rais Kikwete alikuwa na nia njema ya kuwapatia Watanzania Katiba Mpya, lakini wahafidhina wa CCM hawataki wananchi wapate katiba yenye maoni yao.
“Kikwete alikuwa na nia njema ya kuwapatia Watanzania Katiba Mpya, lakini wapo wanachama wa CCM ambao hawataki mabadiliko ili kulinda masilahi yao,” anasema.
Lipumba anadai kuwa Wahafidhina wa CCM wamefanikiwa kumshawishi rais na akaanza kuiponda Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kusababisha mchakato huo kuingia dosari.
“Kwa hiyo ili kujibu swali hilo ni kwamba CCM ndiyo wanaokwamisha upatikanaji wa Katiba Mpya,” anasema.
Kwa upande wake Waziri Wassira anasema wanaokwamisha upatikanaji wa Katiba mpya ni wale wanaojiita Ukawa waliosusia vikao vya bunge kwa kutoka nje ya ukumbi.
“Katiba Mpya haiwezi kujadiliwa katika eneo la Kibandamaiti au katika viwanja vya Jangwani. Katiba inaandikwa bungeni, wenzetu Ukawa wamekimbia,”anasema.
Wassira anasema, “Njooni bungeni tuandike Katiba ili tuwaachie wananchi waamue katika kura ya maoni, wao ndiyo wenye uamuzi wa mwisho.
Wassira anasema Bunge la Katiba lina uwezo kisheria kubadilisha mambo yaliyomo kwenye Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba tofauti na madai ya Ukawa kuwa halina uwezo huo.
“Ni lazima nieleze wazi kwamba Bunge la Katiba haliwezi kupitisha kila jambo lililowekwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, kuna mambo tutayabadilisha na hiyo ndiyo kazi ya Bunge,” anasema Wassira.
Anasema haiwezekani bunge lenye wajumbe 629 liwe na kazi ya kupitisha kila kilichomo kwenye rasimu, vinginevyo uwepo wake hauna maana.
“Kama ni hivyo basi bunge hilo lingeweza kukaa kwa wiki moja na kumaliza kazi hiyo kwa sababu ni kazi rahisi sana,” anasema.
Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu anasema wanaoyapinga maoni ya wananchi yaliyopo kwenye rasimu, ndiyo hawana nia njema na Katiba mpya.
“Katiba ni ya wananchi, huwezi kupuuza maoni yao halafu useme una nia njema ya kutaka Katiba mpya, CCM wanataka Katiba yenye maslahi kwa vigogo wachach,” anasema.
Lissu anasema ili kufanikisha lengo lao,  kati ya wajumbe 201 walioteuliwa kuwakilisha makundi mbalimbali, wajumbe 166 ni wanachama wa  CCM ambao waliteuliwa kwa lengo la kuongeza nguvu.
“Ndiyo maana sisi tumeamua kutoka bungeni ili tusishiriki katika uovu huo, tunafahamu kabisa CCM lengo lao ni kuandaa katiba ile ile lakini yenye rangi tofauti,” anasema.
Wajumbe wa tume
Wajumbe wa  iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Humphrey Polepole na Awadhi Nassor Said, wakasema Wajumbe wa Bunge la Katiba ambao ni wanachama wa  CCM, waliukejeli mchakato huo, hivyo hawana nia njema na mustakabali wa taifa.
Awadhi anasema Tume ya Jaji Warioba ilikusanya maoni ya wananchi katika wilaya 143, ikifanya mikutano 12 katika kila wilaya ya Tanzania bara na 22 Zanzibar, hivyo ikafanya jumla yake kuwa 1,700.
Anasema kulikuwa na mabaraza ya katiba 177 na kwamba asasi za kiraia 614 ziliunda mabaraza ambayo wajumbe wake hivyo wajumbe wake wakafanikisha kupatikana kwa rasimu, iweje misingi yake ipinduliwe na  watu 629.
“Tume ilichukuwa sampuli ya maoni sasa kama wao CCM wanasema wanaotaka serikali tatu ni wachache wao wanataka serikali mbili kwa takwimu zipi,” anasema.
Polepole anaionya CCM juu ya mpango wa uchakachuaji wa rasimu hiyo halisi, huku akiwaasa Watanzania kufuatilia mchakato huo kwa makini.
Mchakato uahirishwe hadi 2016
Wakati huohuo Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), limependekeza  Bunge la Katiba  kuahirishwa hadi mwaka 2016, baada ya uchaguzi mkuu.

0 Comments