HAKI ZA MPANGAJI NA MAJUKUMU YA MWENYE NYUMBA KISHERIA



ufupi
Pia, endapo mwenye nyumba ndani ya miezi sita atakuwa hajafanyia marekebisho basi mpangaji ana haki ya kuvunja mkataba na kudai fidia lakini anapaswa kutoa notisi ya mwezi mmoja kabla ya kufanya hivyo.
 


Ardhi ni kitu muhimu sana katika maisha ya kila siku ya binadamu. Hata hivyo, ukweli ni kwamba siyo kila Mtanzania anamiliki ardhi.

Wengi wamepanga kwenye nyumba au maeneo ya watu wengine.

Wiki iliyopita tuliangalia kwa kina majukumu ya mpangaji, leo tutajikita zaidi kwenye haki za mpangaji na majukumu ya mwenye nyumba.

Sheria inayosimamia haya ni pamoja na ile ya ardhi ya mwaka 1999, sheria ya usajili wa ardhi sura ya 334, kesi mbalimbali, mkataba wa pango pamoja na sheria zingine zote za nchi.

Sheria imeweka haki hizi na majukumu kwa mwenye nyumba na inapaswa ziheshimike. Sheria na majukumu haya zinapaswa kuzingatiwa.

Endapo mpangaji kalipa kodi yake vizuri na anaheshimu mkataba waliojiwekea, ana haki ya kutumia eneo/nyumba hiyo kwa kipindi chote cha muda wa mkataba bila bughudha ya aina yoyote (peaceably and quietly possess and enjoy the land leased). Hii ni kwa mujibu wa kifungu cha 88 (1) (a) cha Sheria ya Ardhi Sura ya 113.

Kupewa taarifa kuhusu upekuzi wowote

Endapo mwenye nyumba anataka kufanya upekuzi wa aina yoyote kwenye nyumba ya mpangaji, anatakiwa na sheria kutoa taarifa hii mapema.

Haki ya kupata nyumba ambayo ipo katika hali nzuri anayoweza kuishi binadamu (fit for human habitation) kwa kipindi chote cha mkataba, kwa hiyo mwenye nyumba ana jukumu hilo kisheria, siyo leo mtu amepanga kesho ukuta umebomoka hiyo nyumba haitakuwa katika hali nzuri. Ni jukumu la mwenye nyumba kuirekebisha. Hii ni kwa mujibu wa kifungu cha 88 (1) (d) cha Sheria ya ardhi Sura ya 113.

Mwenye nyumba kutotumia ardhi ya jirani au sehemu yoyote ya ardhi itakayo athiri matumizi ya ardhi iliyokodiwa; kwa mfano mtu anapanga leo eneo kama sehemu ya kufundishia, baada ya wiki unakuja kufunga mashine jirani na hapo inayopiga kelele muda wote kiasi cha eneo lilipongwa linakuwa halina maana tena.

Mwenye nyumba kufanya matengenezo pale nyumba inapoharibika au kubomoka na kufanya kuwa siyo sehemu ya kuishi binadamu wa kawaida, ikibomoka kwa radi, mvua, mafuriko,upepo mkali n.k. Hii ni kwa mujibu wa kifungu cha 88 (1) (e) cha Sheria ya Ardhi Sura ya 113.

Pia, endapo mwenye nyumba ndani ya miezi sita atakuwa hajafanyia marekebisho basi mpangaji ana haki ya kuvunja mkataba na kudai fidia lakini anapaswa kutoa notisi ya mwezi mmoja kabla ya kufanya hivyo.
Mwenye nyumba pia ana jukumu la kulipa kodi ya jengo na kodi zingine zinazohusiana na nyumba hiyo.Hii ni kwa mujibu wa kifungu cha 88 (1) (g) cha Sheria ya ardhi Sura ya 113. Mfano kodi ya jengo n.k. Bili za umeme na maji na makubaliano baina ya pande mbili mpangaji na mwenye nyumba.
Pia, mpangaji anaweza kuvunja mkataba endapo ataona eneo/ nyumba aliyopanga haifai tena kwa matumizi kama yale ya awali, kwa mfano mtu amepanga kwa ajili ya kuendesha mashine yake lakini baadaye umeme wanakata kwa kosa la mwenye nyumba, kisheria huyu mpangaji hawezi kuendelea na hilo eneo, anaweza kutoa notisi ya mwezi mmoja na kuvunja mkataba.
Kimsingi hizi haki lazima ziwepo kwa kila mkataba, na mikataba lazima iwe imeandikwa kisheria na inayokubalika.
Mwandishi wa makala hii ni Jebra Kambole Wakili wa Kujitegemea kutoka Kampuni ya Law Guards Advocates wa jijini Dar es Salaam.

0 Comments