SERIKALI YAPIGA MARUFUKU KUGAWA KONDOMU MASHULENI

 



Kwa ufupi

Marufuku hiyo imekuja baada ya kubainika kwamba baadhi ya taasisi zinajihusisha na ugawaji kondomu kwa wanafunzi.

Mwanza. Serikali imetoa onyo kwa taasisi zisizo za Serikali kuacha kupandikiza vitanzi na kuwagawia kondomu wanafunzi shuleni kwani wanahamasisha ngono kwa umri mdogo.

Kauli hiyo imetolewa leo Machi 6 na Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Mery Tesha wakati wa maonyesho ya siku mbili ya wanawake katika viwanja vya Ghandh All.

Tesha amesema Serikali imebaini baadhi ya mashirika na taasisi zisizo za Serikali zinazunguka na kutoa huduma hizo shuleni.

“Wanafunzi hawa tuwalee katika maadili mema yanayostahili badala ya kuwapatia kondomu na vitu vingine vinavyohamasisha kufanya ngono, jambo hili halikubaliki hata kidogo,” amesema Tesha.

Mwananfunzi anayetarajia kujiunga kidato cha tano Sada Jabiri ameiomba Serikali kuifuta sheria ya mwaka 1971 ambayo inamruhusu mtoto kuolewa akiwa na miaka kuanzia 15.

“Ili kumjengea mtoto haki ya kujitambua na kutoa uamuzi sahihi ni vyema sheria ingesema hata ianzie miaka 21 ambapo mtoto anakuwa ana ufahamu mkubwa,” amesema Sada.

Mwenyekiti wa baraza la watoto Mkoa wa Mwanza, Neema Theonest alisema katika hali hii ya kuelekea uchumi wa viwanda ifikapo 2025 ni vyema kuimarisha usawa wa kijinsia na uwezeshaji wanawake vijijini.

Neema amewataka wanawake waache kubweteka badala yake wajitume kufanya kazi ili kupandisha uchumi kuanzia ngazi ya familia na kutokomeza umasikini.

Akisoma risala kwa niaba ya wanawake wa Nyamagana, Grace Saiti aliiomba Serikali iendelee kutoa fursa nyingi za ajira kwa wanawake na kuwapatia nyadhifa mbalimbali kwani wanawake wana uwezo wa kuongoza na kusimamia shughuli mbalimbali za maendeleo kiuchumi, kisiasa na kijamii.

Pia amesema  elimu ya masuala ya uzalishaji na uanzishaji wa viwanda ifanyike zaidi kwenye maeneo yote ili mwanamke hata wa kijijini afikiwe na aweze kujiendeleza.

 

0 Comments